Kijana mmoja aliyetambuliwa kwa jina moja la Alphonce, mkazi wa Buza Shule wilayani Temeke jijini Dar es Salaam, anadaiwa kumuua kwa kumchoma visu vitano tumboni na kifuani na kufa papo hapo kijana mwenzake, Tuaje Baina.
Tukio hilo la kitatili lililoacha watu midomo wazi, lilitokea wiki iliyopita ya Krismasi maeneo ya Buza, Wilaya ya Temeke.
Habari zinasema chanzo cha mtu huyo kufanya kitendo hicho cha kikatili ni madai ya kuwa Alphonce aliibiwa vitu vyake vya ndani ikiwemo runinga miezi mitatu na Baina.
Lakini katika hali ambayo ilionekana si ya kawaida, shuhuda mmoja alisema muuaji huyo baada ya kufanya kitendo hicho, alienda mitaani na kutamba kuwa amemuua Baina na bado watu wake wawili nao watarajie kufa ingawaje alikuwa hawataji kwa majina.
Kutokana na kutamba kwake huku akipita katika majumba ya starehe, wananchi walikerwa ndipo muuaji huyo baadaye aliamua kwenda nyumbani kwake ambapo watu wenye hasira walimfuata ili wakamuadabishe.
Habari zinasema wananchi hao walifanikiwa kumpata mtuhumiwa huyo na kumfikisha katika eneo la tukio ambapo alikutwa Baina aliyechomwa visu akiwa mahututi, ndipo walipoanza kumpa kichapo.
Hata hivyo, mtu huyo aliokolewa na polisi wa kituo cha Buza ambao waliwasihi wananchi wasimuue ili akaisaidie polisi kutokana na tukio hilo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Temeke, ACP Engelbert Kiondo akizungumzia suala hilo alisema: “Tunamshikilia Alphonce na tunamchunguza kuona kama ana akili timamu,” alisema Kamanda Kiondo.
Naye aliyekuwa Meneja wa Casino ya Kilimanjaro inayomilikiwa na Hoteli ya Sea Cliff, Rola Cheterolia,42, raia wa kigeni alikutwa amefungwa kwa kamba akiwa hajitambui Desemba 27, mwaka jana na mlinzi kuingia mitini.
Baadaye Mzungu huyo, raia wa Bulgaria alifariki dunia akiwa anakimbizwa katika Hospitali ya Hindu Mandal. Kifo chake kimeacha mshituko mkubwa hasa baada ya askari mlinzi aliyekuwa zamu siku hiyo kutoroka na kwenda kusikojulikana.
Mwili wake ulihifadhiwa kwenye hospitali hiyo kwa ajili ya uchunguzi.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi, Kinondoni ACP Charles Kenyela alisema marehemu alikutwa amefungwa kamba mikononi na miguuni, hali ambayo inaonesha alinyongwa na upelelezi unaendelea.
Aidha katika tukio lingine, mtu aliyefahamika kwa jina la Andrew Charles, 34, Mkazi wa Magomeni Makuti amekutwa amekufa akiwa hana jeraha lolote, mwili wake ukiwa katika gari aina ya Benzi lenye namba za usajili T 585 AFP.
Taarifa za kipolisi kutoka kwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Charles Kenyela zinasema kuwa Andrew alikutwa amefariki akiwa ndani ya gari hilo ambalo hata hivyo, halitembei kwa kuwa ni bovu na limeegeshwa kwa muda mrefu.
Aidha, Kamanda Kenyela asema kuwa uchunguzi wa kina kuhusiana na tukio hilo unaendelea ili kubaini ukweli wa kifo hicho.
Kaka wa Andrew aliyejitambulisha kwa jina Keneth Charles alisema hajui kilichomsibu mdogo wake hadi akafariki dunia.
Siku chache kabla ya Krismasi, kifo kingine kilitokea baada ya Afisa wa Takukuru, Bhoke Ryoba kupigwa risasi kichwani na mfanyakazi mwenzake wakiwa kwenye sherehe.